JERRY MURO: HAKUNA WA KUNIPUNGUZA KASI
Afisa Habari wa Yanga Jerry Muro amesema, hakuna mtu wa kumpunguza kasi isipokuwa mwajiri wake.
Jerry ametoa kauli hiyo wakati akihojiwa na kituo kimoja cha radio cha jijini Dar es Salaam kuhusiana na hukumu ya kufungiwa mwaka mmoja kutojihusisha na soka iliyotolewa na TFF.
“Mwajiri wangu aliyekuwa akinituma nipambane akikubali nikae pembeni, nitakaa pembeni. Ndiyo maana nasema, mimi nitamsikiliza mwajiri wangu akiniambia nikae pembeni nitaa pembeni lakini hawa wengine wote, hakuna wa kunipunguza kasi.”
Lakini paia Muro amesema hatambui hukumu hiyo kwasababu hakupewa haki yake ya msingi ya kusikizwa.
“Kwanza mimi sitambui hicho kifungo na sikubaliani nacho, kuna kitu kimoja nadhani wamesahau. Kuna kitu kinaitwa ‘principle of natural justice’ (misingi ya haki ya mtu kusikilizwa), sasa mimi niwaambie wana Yanga, nitarejea Jumatatu kutoka kijijini Machame na tutaongea na nitatoa tamko lakini sikubaliani na hiyo adhabu.”
“Hata kama wanasema wamenifungia nataka niwakumbushe, wanamambo mengi na hawakuyafanya na kama wanaona mimi kipaumbele nitarudi Dar es Salaam halafu tutawajibu kwa kishindo wajue sisi ndiyo Yanga.
Kuhusu suala la kukata rufaa Muro alikuwa na msimamo huu: “Sikati rufaa, na kuwaonesha kwamba sikati rufaa, narudi na tutawajibu kwa kishindo kikuu. Mimi sijaajiriwa na TFF, mwajiri wangu akiniambia nikae pembeni nitakaa lakini siyo mtu wa pembeni. Kwahiyo mimi nasubiri taarifa kutoka kwa mwajiri wangu, kama mwajiri wangu hatanipa taarifa hii inaitwa kanyaga mwendo nitafanya kazi yangu wakitaka waifungie Yanga.”
Kamati ya maadili ya TFF imetangaza kumfungia Muro kutojihusisha na masuala ya soka kwa kipindi cha mwaka mmoja pamoja na kumtoza faini ya shilingi milioni tatu kutokana na madai ya kupingana na maagizo ya shirikisho hilo pamoja na kulishambulia kupitia vyombo vya habari
No comments: